Bibi alikanusha madai dhidi yake akisema alikuwa tu anabishana na wanawake wengine kuhusu maji

Mahakama nchini Pakistan imesesema adhabu ya kifo iliyotolewa kwa mwanamke mkristo aliyeshtakiwa kwa kukufuru dini mwaka 2010 itatekelezwa.

Asia Bibi alipatikana na hatia ya kutoa matamshi ya kukera na kuudhi kumhusu Mtume Mohammad wakati akibishana na mwanamke mwingine muislamu.

Mahakama kuu mjini Lahore, ilikataa rufaa yake dhidi ya hukumu aliyopewa na mahakama ya chini. Mawakili wake wameahidi kuwasilisha kesi hiyo katika mahakama ya juu zaidi nchini humo.

Hukumu iliyotolewa dhidi ya Bibi mwaka 2010 ilizua mjadala mkubwa kimataifa.
Wanasiasa wawili wenye ushawishi waliuawa mwaka uliofuata baada ya kutoa wito wa kubadilishwa kwa sheria dhidi ya kukufuru wakati kesi ya Bibi ilipokuwa inaendelea.

Bibi alikanusha madai dhidi yake akisema kuwa mabishano yalitokea kati ya kikundi cha wanawake kuhusiana na nyungu ya maji.

Kukufuru au kutoa matamshi ya kuudhi dhidi ya dini ya kiislamu ni swala tete sana nchini Pakistan. Wakosoaji wanasema sheria dhidi ya kukufuru hutumiwa vibaya na baadhi ya watu tofauti zinapoibuka na kwamba jamii zilizotengwa ndizo hulengwa zaidi.

Tangu mwaka 1990, idadi kubwa ya wakristo wamefungwa jela kwa kukufuru au kukejeli dini ya kiislamu.

Wengi wao wamehukumiwa kifo na mahakama za chini huku nyingi ya hukumu zikifutiliwa mbali na mahakama za juu kwa kukosekana ushahidi wa kutosha.

CHANZO: BBC