Tuesday, September 15, 2015

Tuesday, September 15, 2015
Australia inaelekea kupata waziri mkuu mpya baada ya Tony Abbott (pichani kulia) kuondolewa madarakani katika chama cha Liberal na mmoja wa mawaziri wa chama chake.

Kwenye uchaguzi wa kiongozi wa chama uliofanywa haraka, Bw Abbott, ambaye umaarufu wake umekuwa ukididimia kwa mujibu wa kura za maoni, alipata kura 44 huku waziri wake Bw Malcolm Turnbull akipata kura 54.

Wabunge wa chama hicho hata hivyo walimpigia kura Julie Bishop kusalia kama naibu kiongozi wa chama hicho.

Bw Turnbull anatarajiwa kuapishwa baada ya Bw Abbott kumwandikia gavana mkuu na kujiuzulu.

Mapema Jumatatu, kwenye kikao na waandishi wa habari, Bw Turnbull alisema iwapo Bw Abbott angesalia kama kiongozi wa chama hicho, serikali ya muungano ingeshindwa kwenye uchaguzi mkuu ujao.

Alisema ilikuwa vigumu kwake kufanya uamuzi huo, lakini kwamba ni “wazi kuwa serikali haijafanikiwa katika kutoa uongozi wa kiuchumi unaohitajika” na kwamba Australia inahitaji mtindo mpya wa uongozi.

Bw Turnbull atakuwa waziri mkuu wa nne wa Australia tangu 2013.

Waziri mkuu wa chama cha Leba Julia Gillard aliondolewa uongozini na Kevin Rudd kwenye kura ya uongozi wa chama Juni 2013, miezi kadhaa kabla ya uchaguzi mkuu ambao chama cha Liberal, chake Tony Abbott, kilishinda.

Bi Gillard mwenyewe alikuwa amemuondoa Rudd kama waziri mkuu 2010.

0 comments: