Tuesday, October 7, 2014

Tuesday, October 07, 2014

Chama cha APPT- Maendeleo, kimepongeza kupitishwa kwa Rasimu ya Katiba inayopendekezwa katika hatua ya Bunge Maalum la Katiba na kuahidi kupigania suala la mbunge kuwajibishwa na wananchi liingizwe katika katiba anaposhindwa kutekeleza majukumu yake badala ya kusubiri miaka mitano.
Katibu Mwenezi wa Taifa wa chama hicho, Godfrey Davis, akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, alisema APPT- Maendeleo kimechukua hatua ya kupongeza Rasimu hiyo kwasababu mambo mengi yanayohusu wananchi na wanasiasa yameingizwa katika katiba hiyo.
“APPT Maendeleo tangu awali tulitoa mapendekezo kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwamba  Rais ili aweze kutangazwa mshindi apate zaidi ya asilimia 50, mgombea binafsi awepo, Tume Huru ya Uchaguzi na suala la matokeo ya Rais yahojiwe mahakamani, yote haya yameingizwa kwenye Rasimu ya Katiba.
Hivyo tuna sababu ya kupongeza hatua hii,” alisema.Davis alisema wanasiasa na wadau wengine wanaopinga Rasimu ya Katiba hiyo watambue kuwa  hiyo siyo ya mwisho kwani kutakuwa na kipindi cha mpito mambo mengine ambayo hayajaingizwa  yataingizwa  siku  za  mbeleni.
Alisema pamoja na kupitishwa mambo mazuri katika Rasimu ya Katiba inayopendekezwa, APPT- Maendeleo kitaendelea kupigania suala la wananchi kuwa na mamlaka ya kuwajibisha wabunge wao ili kuleta uwajibikaji mzuri.
Katibu Mwenezi huyo alisema kuingizwa kwa kipengele hicho katika katiba kutasaidia wabunge kuwa makini katika utekelezaji wa majukumu yao ya kuwaletea maendeleo wananchi badala ya hivi sasa ambapo baadhi ya wabunge wamekuwa wakiwatelekeza wapiga kura wao kwa muda mrefu na kuonekana wakati wa uchaguzi mkuu tu.
Aliongeza kuwa mambo mengine ambayo chama hicho kitaendelea kupigania ni suala la mawaziri kutotokana na wabunge, mgombea ubunge awe na elimu kuanzia kidato cha nne, Bunge liwe na chemba mbili yaani wabunge wa Tanzania na wabunge wa Tanzania bara.
Davis ameiomba serikali nakala za rasimu ya mwisho zitolewe nyingi na kwa wakati ili wananchi wapate fursa ya kuisoma na kutoa mawazo yao kabla ya kuchukua uamuzi wa kupiga kura ya maoni.

CHANZO: NIPASHE     

0 comments: