Sunday, April 5, 2015

Sunday, April 05, 2015
                           

Kisarawe. Hofu imewakumba waumini wa Kanisa Katoliki la Mtakatifu Stephano, Kisarawe mkoani Pwani katika ibada ya Ijumaa Kuu baada mtu mmoja kukamatwa katikati ya ibada ya Ijumaa Kuu akiwa na bastola yenye risasi nane.

Kwa mujibu wa habari zilizopatikana kutoka kwa waumini na kuthibitishwa na polisi, mwanaume huyo ambaye si muumini wa kanisa hilo anadaiwa kutaka kufanya uhalifu kanisani hapo na alikamatwa baada ya waumini kushtukia mienendo yake isiyo kuwa ya kawaida.

Tukio hili limetokea katika kipindi ambacho kuna tishio la uhalifu unaohusishwa na ugaidi katika maeneo mbalimbali nchini, ambapo kuna uporaji wa silaha unaofanywa na watu wasiojulikana baada ya kuwaua polisi.

Miongoni mwa matukio hayo, mawili yametokea mkoani Pwani na la hivi karibuni la Kongowe, limetokea mpakani mwa Dar es Salaam na Pwani.

Vilevile tukio hili limetokea wakati waumini hao hawajasahau mauaji ya kutisha nchini Kenya ambako magaidi wamevamia Chuo Kikuu cha Garissa na kuua wanafunzi 147.

Kutokana na hofu ya kiusalama, makanisa mbalimbali katika kipindi hiki cha sikukuu yameongeza ulinzi na katika baadhi ya makanisa ni marufuku kuingia mikoba au vifaa vingine visivyoeleweka.

Kwa mujibu wa waumini wa kanisa hilo, tangu alipoingia kanisa na ibada ilipokuwa inaendelea yeye, alikuwa anaonekana kufanya mawasiliano ya simu mara kwa mara, kinyume na kanuni za ibada kanisani humo.

Waumini hao walisema mtu huyo aliwahi kabla ya muda wa ibada na kuketi katika viti vya nyuma, lakini baadaye alikuwa anahamahama na wakati mwingine alitoka nje kufanya mawasiliano.

“Unajua sisi Wakristo tunajuana na kama mgeni pia ataonekana mgeni kikanisa, lakini siyo kinidhamu, maana nidhamu ya ibada inalingana katika makanisa yote. Lakini huyu jamaa alikuwa na pilika nyingi, mara atoke nje, anaongea na simu, mara atume ujumbe wa simu, kweli alionekana tofauti kabisa,” kilisema chanzo chetu.

“Tukiwa katikati ya ibada, mtuhumiwa alimwomba muumini mmoja wa kike aliyekuwa jirani naye amwonyeshe choo kilipo, akatoka nje lakini kwa kuwa waumini walikuwa wanamwona tofauti, walimfuatilia na kukuta hajaelekea chooni alikoelekezwa, bali alijibanza ukutani na kuongea na simu huku akiingiza mkono ndani ya koti,” aliongeza muumini huyo.

Wakati mtu huyo akiwa nje, ilitolewa taarifa Kituo cha Polisi kilichopo karibu na askari walifika kanisani hapo na kumkamata.

0 comments: