Wednesday, August 19, 2015

Wednesday, August 19, 2015

 
Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es salaam imethibitisha uwepo wa ugonjwa wa kipindupindu ambapo hadi sasa wagonjwa watatu wameripotiwa kupoteza maisha huku zaidi ya 34 wakiwa wamelazwa katika vituo vya Mwananyamala na Mburahati jijini Dar es Salaam.
Wataalamu wa afya wanasema mazingira yanayozunguka makazi ya kuishi ndiyo yanaweza kusababisha uwepo wa magonjwa ya maambukizi kama kipindupindu huku ikisisitizwa, kula bila kunawa, kula matunda hovyo, kutoka msalani bila kunawa,kunywa maji bila kuchemsha na kugusana na mgonjwa wa kipindupindu ni kati ya sababu kuu zinazosambaza ugonjwa huu. Ikiwa ni siku moja tu baada ya kuripotiwa kuingia kwa ugonjwa huu, mpangaji mmoja ambaye mwanae amepatwa na ugonjwa huo, ametishiwa kufukuzwa anakoishi baada ya mwenye nyumba kuhofia huenda familia yake ikakubwa na ugonjwa huo. 
Jitihada mbalimbali zinachukuliwa kuwaokoa wagonjwa wa kipindupindu katika hospitali za Mwananyamala na Mburahati na wauguzi wameendelea kuwasisitizia wananchi kuzidisha usafi hasa kipindi hiki cha mlipuko wa ugonjwa huu wa kipindupindu.
Mganga Mkuu wa Manispaa ya Kinondoni Dkt Azizi Msuya amesema hadi sasa wamekwisha sambaza dawa katika kata zaidi ya 70 zinazozunguka kambi hizo ikiwa ni pamoja na kupulizia dawa za kuulia vijidudu vya ugonjwa huo.
Kwa upande mwingine, Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni Mhandisi Mussa Natty, amewatahadhalisha wakazi wa manispaa hiyo kuepukana na misongamano pamoja na kula chakula cha pamoja ili kuweza kuepuka uwezekano wa kupata maambukizi ya ugonjwa huo.
Mpaka sasa zaidi ya wagonjwa 34 wamelazwa, mwananyamala ikiwa na wagonjwa 18 wakubwa wanne na watoto 14. Kituo cha sinza kina wagonjwa 16 ambapo kati yao wanaume ni 13 wanawewake 3.

0 comments: