Mshauri mashuhuri wa shirika la Afya duniani WHO ameonya kuwa visa vipya vya ugonjwa wa Ebola vinatarajiwa miongoni mwa maafisa wa afya hata katika mataifa yaliostawi kiuchumi kutokana na mifumo ya afya ya kisasa.

Profesa Peter Piot amesema kuwa hashangai kwamba muuguzi mmoja wa Uhaspania aliambukizwa ugonjwa huo.Muuguzi huyo ni mtu wa kwanza anayejulikana kuambukizwa ugonjwa huo nje ya eneo la Afrika Magharibi.Aliwatibu wamishenari wawili ambao walifariki kutokana na ugonjwa wa Ebola mjini Madrid.

Wauguzi katika hospitali ya Madrid
Muuguzi huyo anayefahamika katika vyombo vya habari kama Teresa Romero,aliwauguza wawili hao baada ya kuhamishwa kutoka Afrika Magharibi.
Anaendelea kuhudumu katika karantini katika mji mkuu wa Uhispania pamoja na mumewe na watu wengine watatu.
Watu wengine hamsini kutoka Uhispania pia wanachunguzwa.
Muuguzi huyo aliliambia gazeti la El Mundo siku ya jumatano kwamba alifuata maagizo na hajui ni vipi aliambukizwa.
Amesema kuwa ijapokuwa anajihisi vyema kiafya anasikia uchovu.


Muuguzi aliyeambukizwa Ebola nchini Uhispania
Mtu wa tano kuwekwa katika karantini-ambaye anaripotiwa kuwa rafiki ya nesi huyo na ambaye pia ni mmoja ya wanachama wa maafisa wanaosimamia maambukizi ya Ebola katika hospitali hiyo alilazwa siku ya jumatano akiwa na homa.
Mwandishi wa BBC Lucy Williamson mjini Madrid anasema kuwa maafisa wa afya katika hospitali hiyo walikuwa na wasiwasi mkubwa kazini siku ya jumanne,huku wengine wakilia na wengine kuondoka katika jumba hilo la afya.
Vyombo vya habari nchini Uhispania vinasema kuwa majirani wa muuguzi aliyeambukizwa wamekuwa wakitafuta huduma za dharura,wakitaka kujua vile wanavyoweza kuwalinda wana wao baada ya kutumia lifti na maeneo mengine ya hadhara.
Katika kisa chengine mume wa mwanamke huyo ameripotiwa kutafuta agizo la mahakama la kumtenga mbwa wao ambaye huenda pia ameambukizwa ugonjwa huo.
Hatahivyo wanaharakati wa wanyama wameikosoa hatua hiyo wakisema kuwa hakuna ushahidi kwamba ugonjwa wa Ebola unaweza kusambazwa na mbwa.

CHANZO: BBC