Thursday, October 2, 2014

Thursday, October 02, 2014

Mkurugenzi Mtendaji wa zamani wa Shirika la Umeme Tanzania (Tenesco), William Mhando

Mahakama imeelezwa kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa zamani wa Shirika la Umeme Tanzania (Tenesco), William Mhando, hakuwa miongoni mwa wajumbe walioshughulikia mchakato wa zabuni iliyopewa kampuni inayomilikiwa na mkewe kusambaza vifaa vya ofisi katika shirika hilo.
Shahidi wa upande wa mashitaka, Athanas Kalikamwe, alidai mbele ya Hakimu Frank Moshi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jana kuwa wajumbe waliohusika katika mchakato huo ni wale waliotoka katika timu ya upembuzi na bodi ya tenda.
Alidai kuwa katika taasisi hizi mbili zinazojitegemea, Mhando hakuwa miongoni mwa wajumbe na kuwa mshitakiwa alihusika katika hatua za mwisho za utiaji saini wa mkataba huo uliotolewa kwa kampuni ya Santa Clara Supplies Company Limited.
Kalikamwe alikuwa akihojiwa na upande wa utetezi ukiongozwa na mawakili Daniel Ngudungi, Alex Mgongolwa, Jamhuri Johnson na Augustine Kusalika wakati wa kusikiza kesi ya matumizi mabaya ya madaraka inayomkabili Mhando, mkewe Eva na watumishi wengine wa Tanesco.
Alidai kuwa kama mfanyakazi wa Tanesco, ambayo ni taasisi ya serikali angepaswa kutangaza maslahi kama angegundua kuwa mmoja wa wazabuni walioomba angekuwa ndugu yake.
Alidai kuwa waliohusika na mchakato wote kutoka bodi ya tenda na upembuzi walipaswa kutangaza maslahi kwenye vikao vyao kama wangebaini kuwa wana uhusiano na kampuni hiyo.
Akiongozwa na Mwendesha Mashikata kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Leonard Swai, shahidi huyo aliwasilisha taarifa ya upembuzi wa tenda hiyo na nyaraka zingine kama ushahidi kwenye shauri hilo.
Washitakiwa wengine katika shauri hilo ni France Mchalange na Sophia Misidai, ambao wote ni wahasibu waandamizi na Naftali Kisinga, ambaye ni afisa ugavi.
 

0 comments: