Wednesday, April 1, 2015

Wednesday, April 01, 2015
                        
Mahakama ya Wilaya ya Dodoma imerudishia dhamana mwenyekiti wa jumuiya ya wafanyabiashara nchini Johnson Estomii Minja na kutupilia mbali hoja za zilizotolewa na upande wa mashitaka kuwa mwenyekiti huyo alikiuka masharti ya dhamana kwa kufanya mikusanyiko na kushawishi wafanyabiashara kuendelea kugomea matumizi ya EFD na kufunga maduka.

Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Dodoma Rhoda Ngimilanga ameyakubali maombi ya dhamana kwa mwenyekiti huyo baada ya kupitia hoja za pande mbili za mashtaka na utetezi.  
Awali akiwasilisha hoja kwa upande wa mashtaka, Wakili wa Serikali Bi.Rose Shio aliiambia mahakama hiyo kuwa mnamo tarehe 28 mwezi wa kwanza mwaka huu mshtakiwa alifanya mkutano na wafanyabiashara katika eneo la Imagi mjini Dodoma,ambapo pamoja na mambo mengine alishawishi wafanyabishara kugoma kutumia mashine za EFDs, kugoma kufungua maduka na kuchochea vitendo vya uvunjifu wa amani.
Hoja hizo zilipingwa vikali na mawakili wa mshitakiwa,ambao ni Godfrey Wasonga na Juma Malima ambao wote kwa pamoja waliieleza mahakama kuwa dhamana ni haki ya mshtakiwa kwa mujibu wa ibara ya 13 (6) b inayosomeka sambamba na ibara ya 15 (1)  ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu haki ya mshitakiwa kutochukuliwa ana hatia mpaka itakapothibitishwa.
Mapema kabla ya Bwana Minja kuwasili katika viwanja vya mahakama umati mkubwa wa wafanyabiashara ulifurika huku ulinzi ukiimarishwa maradufu ndani na nje ya viwanja hivyo sambamaba na shughuli zingine za mahakama kusimama kwa muda.

0 comments: